Ray C atoa kauli nzito asema najuta kujuana na Lord Eyez piaawataja mastar wengine wanaotumia madawa


TUNAENDELEA na mahojiano na staa mkubwa wa Bongo Fleva, Rehema Chalamila ‘Ray C’ ambaye amepona kutoka kwenye uraibu wa matumizi ya madawa ya kulevya. Wiki iliyopita alifunguka mambo mengi ambapo tuliishia pale alipokuwa akizungumzia wimbo wake wa mwisho kabla ya matatizo. SONGA NAYO…

Lord Eyez


WIMBO WAKO WA MWISHO KABLA YA MATATIZO NI UPI?

“Ni Moto Moto niliofanya na akina Red Sun na Nonini wa Kenya. Sikuupeleka redioni nchini Tanzania lakini ukiingia mtandaoni kwenye You Tube utaona umesikilizwa na kutazamwa na mashabiki zaidi ya  348,142 hadi sasa.

BAADA YA KUTANGAZA KUATHIRIKA NA KUACHA MADAWA YA KULEVYA, NINI KINAKUTESA?

“Hakuna, najikubali najisikia amani. Nimetua mzigo mkubwa. Watu wananipongeza kwa ujasiri wangu. Hawanitengi, wananipa sapoti sana. Unajua watu wengi hawapendi kujitangaza wakiogopa kunyanyapaliwa. Mimi nilijikubali nikasema bora kusema ukweli ili kuokoa kizazi hiki kinachoangamia kwa madawa ya kulevya. Na kweli suala la madawa ya kulevya limekuwa ishu kubwa nchini. Nafurahi kuwa sehemu ya ukombozi wa jamii ya dunia hii. Siogopi. Kwangu ni tofauti. Mashabiki wangu wananipenda, wananipongeza mitandaoni. Nimepona na maisha lazima yaendelee.

ULIINGIAJE KWENYE MADAWA YA KULEVYA?

“Kuna mtu alikuwa akiniwekea bila mimi kujua, sitaki kukumbuka hiyo kitu kitu. Mwanzoni ilikuwa raha lakini baadaye ikawa karaha na balaa kubwa. Nilikuwa mtu mwenye malengo.

NI NANI ALIKUINGIZA KWENYE MATUMIZI YA MADAWA YA KULEVYA?

“Nilishasema ni aliyekuwa boyfriend wangu, (anamtaja). Ni Lord Eyez. Nilimpenda sana lakini najuta kumjua. Arusha wananipenda, wananiita shemeji. Naahidi kwenda Arusha kuwapa burudani. Nami nawapenda. Niliachana naye mwaka 2010 baada ya kuona hali inazidi kuwa mbaya. Nilimwambia nampenda lakini ilibidi tuachane. Hakukuwa na namna nyingine. Nilikuwa sijui kama lile jambo linaweza kuharibu maisha yangu. Mwanzoni alikuwa akiniwekea bila mimi kujua. Nikaona bora niachane naye ninusuru uhai wangu. Nilikwenda Nairobi lakini haikusaidia.

ULIKUTANA LINI NA LORD EYEZ?

“(anawaza) Kama sikosei ni mwaka 2008 na tuliachana mwaka 2010.”

UHUSIANO WAKO NA LORD EYEZ UKO KWA SASA?

“Tulikuwa tukionana tunasalimiana. Sijakutana naye muda mrefu lakini sina ugomvi naye. Hata tukikutana nitamsalimia vizuri kabisa. Simchukii ila nachukia madawa ya kulevya. Kama bado anatumia namuombea kwa Mungu aache. Wenzetu wengi wamekufa, narudia tena, Mungu amnusuru kama bado anatumia.”

ILIKUWAJE UKASAIDIWA NA JK?

“Baada ya ninyi (Global kupitia Gazeti la Ijumaa) kuandika kuhusu mimi ndipo Daddy (Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete) akanisaidia, namshukuru sana kwa kweli. Pia namshukuru Ruge kwa namna alivyonipigania. Mungu atamlipa.”

UNAWAJUA VIZURI WASANII WANAOTUMIA MADAWA YA KULEVYA, UNAWEZA KUWATAJA AU UNAWAAMBIA NINI?

“Nawajua (anamtaja msanii mkubwa wa kiume wa Hip Hop Bongo). Anasema hawezi kuacha lakini mpenzi wake anatumia dozi ya kuacha madawa ya kulevya. Yeye anamkatisha tamaa. (anawataja wengine) Nawasihi waache watakufa. Dawa ya kuacha ipo na siyo nje ya nchi, ni Muhimbili (Hospitali ya Taifa, Dar) tu na huduma inatolewa vizuri sana. Mimi nimepona kwa nini wao wasipone?”

RAY C KWELI UMEPONA?

“Bado naendelea na dozi. Nimepona lakini si unajua ile kitu inahitaji muda ili kuwa fiti kabisa?”

MARAFIKI ZAKO NI WATU WA AINA GANI?

“Sina tena zile kampani za madawa ya kulevya. Nina marafiki wa tofauti kabisa. Ni watu ambao hawana hizo ishu kabisa.”

UNA HARAKATI ZOZOTE ZA KUHAMASISHA WATU KUACHA MADAWA YA KULEVYA?

“Nafanya sana. Mtu yeyote nikikutana naye namwambia madhara ya hiyo kitu. Juzi tu niliweka picha mtandaoni nikiwa na wenzangu walioacha madawa ya kulevya. Kweli wapo vizuri na nitaendelea kufanya hivyo ndani na nje ya nchi. Tanzania bila madawa ya kulevya inawezekana.”

BAADA YA MATATIZO RAY C UMEOKOKA?

“No! Hapana. Mimi ni Mkatoliki lakini nimebatizwa na maji mengi katika kanisa analosali mama yangu la Sloam lililopo Mbezi Beach, Dar. Siyo kwamba Katoloki hakuna Mungu ila napenda sana mahubiri ya Sloam. Yananifariji sana.”

UNAPOWAONA WASANII ULIOKUWA NAO LEVO MOJA WAMEFANIKIWA UNAJISIKIAJE?

“Nina mafanikio makubwa. Watu wengi wanadhani mafanikio ni kuwa na mali nyingi. Kwangu ni tofauti. Kuwa na amani tu ni mafanikio makubwa. Hainipi shida kabisa kuona wao wamefanikiwa badala yake nainjoi sana.”

RAY UNA MCHUMBA?

“Hapana na sihitaji. Kwa sasa najipanga kwanza kwa kazi yangu nzuri ya muziki.”

UNAWAAMBIA NINI WAREMBO JUU YA UCHAGUZI WA WAPENZI WA KUWA NAO?

“Unaweza kuzaliwa mtakatifu lakini ukafa mwenye dhambi bila kutegemea. Chondechonde wanawake wenzangu, muwe makini katika kuchagua aina ya wapenzi mnaotaka kuwa nao maishani la sivyo mtaingia kwenye majanga makubwa. Mimi nimepita huko ‘so’ chukua hatua.

No comments: